MFUMO WA UHIFADHI DATA, NISHATI JADIDIFU KUANZISHWA
Mtaalam kutoka Sehemu ya Nishati Jadidifu-
Idara ya Nishati, Wizara ya Nishati na Madini, Mhandisi Stephan
Kashushura (kushoto) akizungumza na mtaalam kutoka kampuni ya vifaa vya
umeme jua ya Mobisol, Devis Mtete (kulia) mjini Kahama mkoani Shinyanga
tarehe 11 Januari, 2017
Mtaalam kutoka kampuni ya vifaa vya umeme
jua ya Zola, Omary Raymond (katikati) akielezea shughuli za kampuni yake
kwa Mtaalam kutoka Sehemu ya Nishati Jadidifu- Idara ya Nishati, Wizara
ya Nishati na Madini, Mhandisi Stephan Kashushura (kulia). Kushoto ni
Msimamizi wa Mradi wa Kuwajengea Uwezo Wataalam wa Nishati na Tasnia ya
Uziduaji (CADESE) chini ya Wizara ya Nishati na Madini, Paul Kiwele
…………
Na Mwandishi wetu, Kahama.
Wizara ya Nishati na Madini kupitia Mradi wa Kuwajengea Uwezo Wataalam wa Nishati na Tasnia ya Uziduaji (CADESE: Capacity Development in the Energy Sector and Extractive Industries), inatarajia kuanzisha mfumo wa uhifadhi data kwa ajili ya nishati jadidifu ujulikanao kama Tanzania Renewable Energy Management Information System (TREMIS) utakaowezesha wawekezaji ndani na nje ya nchi kubaini fursa za uwekezaji zilizopo katika sekta ya nishati jadidifu.
Hayo yameelezwa na Msimamizi wa Mradi wa Kuwajengea Uwezo Wataalam wa Nishati na Tasnia ya Uziduaji (CADESE), Paul Kiwele katika ziara ya maandalizi ya mfumo huo jana, Kahama mkoani Shinyanga
Kiwele alisema katika mfumo huo kutawekwa taarifa mbalimbali kuhusu, tafiti mbalimbali na fursa za uwekezaji katika nishati jadidifu , sera, sheria na taratibu ili kuvutia wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi.
“ Kupitia mfumo huu kutakuwa hakuna haja ya mwekezaji kutoka nje ya nchi kufunga safari hadi Tanzania kwa ajili ya kupata taarifa, taarifa zote zitakuwepo katika mfumo huu utakaounganishwa na tovuti ya Wizara ya Nishati na Madini.
Akielezea maandalizi ya mfumo huo, Kiwele alisema kazi ya maandalizi ya taarifa kwa ajili kuwekwa kwenye mfumo huo imeshaanza kwa kushirikiana na Kitengo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano kutoka Wizara ya Nishati na Madini pamoja na kuzungumza na wauzaji na waendelezaji wa vifaa vya nishati mbadala katika wilaya ya Kahama, Shinyanga kwa ajili ya kupata taarifa zao.
Aliongeza kuwa kutakuwa na warsha itakayokutanisha wadau mbalimbali wa nishati mbadala ili kupata maoni yao kuhusu taarifa zitakazojumuishwa katika mfumo huo.
Mradi wa CADESE unaofadhiliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulika na Maendeleo (UNDP) ulianzishwa mwaka 2014 na unatekelezwa na Wizara ya Nishati na Madini kwa kushirikiana n a wadau wengine kama Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Taasisi ya Uongozi na Taasisi ya Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii (ESRF).
Post a Comment